Friday, April 10, 2015

Mtanzania Anayetuhumiwa Kwa Ugaidi Kenya Kumbe Alitoroka Shuleni Dodoma Tangu Novemba Mwaka Jana



Mtanzania aliyekamatwa Kenya akidaiwa kufanya ugaidi katika Chuo Kikuu cha Garissa uliosababisha vifo vya watu 148, Rashid Charles Mberesero (20) ni mwanafunzi wa kidato cha tano, lakini uongozi wa shule anayosoma umesema alitoweka shuleni hapo Desemba Novemba 2014.
 
Habari zilizothibitishwa na wazazi wake ni kuwa mwanafunzi huyo anasoma katika Shule ya Sekondari ya Bihawana, Dodoma, baada ya kufaulu katika Shule ya Sekondari Gonja mkoani Kilimanjaro.
 
Mama mzazi wa kijana huyo, Fatuma Ali alisema jana kuwa: “Baada ya kufaulu alichaguliwa kujiunga na Sekondari ya Bihawana na likizo alirudi nyumbani na baada ya likizo kuisha aliniaga anarudi shuleni.”
 
Taarifa hizo zimekuja wakati Mberesero maarufu kwa jina la Rehani Dida, akitarajiwa kufikishwa mahakamani leo jijini Nairobi baada ya watuhumiwa wengine kufikishwa mahakamani juzi.
 
Mwendesha mashtaka, Daniel Karuri alisema, “Rehani Dida” hakufikishwa kortini kwani alikuwa na wapelelezi mjini Garissa kukusanya ushahidi zaidi, baada ya kukiri kuwa ni mfuasi wa kundi la Al-Shabaab.
 
Mtanzania huyo anadaiwa kukamatwa baada ya kujificha kwa saa nane akiwa amejichanganya na maiti, lakini baadaye alipanda na kujificha darini akiwa na mabomu.
 
Kauli ya wazazi
Jana, mama huyo, aliwaambia  waandishi wa habari kuwa haelewi ni nani aliyemshawishi mwanaye kujiunga na kundi hilo na kwamba jambo hilo limemshtua.
 
“Hizi taarifa tumezisikia na kuona kwenye TV na kwa kweli zimetushtua sana, mimi nahisi huko shule ndiko alikokutana na watu wabaya,” alisema Fatuma ambaye ni mkazi wa Gonja wilayani Same.
 
Baba mzazi wa mtuhumiwa huyo, Charles Mberesero Temba, alikiri kuwa Rashid ni mtoto wake ambaye alizaa na Fatuma mwaka 1994 na miaka yote alikuwa akiishi na mama yake.
 
“Huyo mtoto sijawahi kuishi naye, muda wote tangu 1994 alikuwa akilelewa na mama yake,” alisema Temba na kuongeza kuwa hakuwahi kuishi na mzazi mwenzake huyo.

No comments:

Post a Comment